SIMBA SC YAFA KIUME MOROCCO, YATOLEWA KWA MATUTA


SAFARI ya Simba SC katika Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mara nyingine leo imeishia hatua ya Robo Fainali baada ya kutolewa na mabingwa watetezi, Wydad Club Athletic kwa penalti 4-3 usiku huu Uwanja wa Mohamed V Jijini Casablanca, Morocco.
Dakika 90 zilimalizika kwa Wydad AC kushinda 1-0, bao pekee la mshambuliaji Msenegal, Bouly Junior Sambou dakika ya 24 kwa kichwa na kufanya sare ya jumla ya 1-1 kufuatia Simba kushinda 1-0 kwenye mchezo wa kwanza wiki iliyopita Dar es Salaam, bao la mshambuliaji Mkongo Jean Othos Baleke dakika ya 31.
Na katika mikwaju ya penalti, shujaa wa Wydad alikuwa ni kipa Youssef El Motie ayeokoa penalti mbili za beki Shomari Kapombe na kiungo Clatous Chama.
Waliofunga penalti za Wydad ni kiungo Yahya Jabrane, mabeki Ayoub El Amloud, Amine Aboulfath na kiungo Abdellah Haimoud wakati waliofunga za Simba ni viungo Erasto Nyoni, Mrundi Said Ntibanzokiza na mshambuliaji Mzambia, Moses Phiri.
Sasa Wydad itakutana na mshindi wa jumla katí ya CR Belouizdad ya Algeria na Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini zinazorudiana Jumamosi Uwanja wa Loftus Versfeld mjini Pretoria. 
Mechi ya kwanza Mamelodi ilishinda 4-1 Uwanja wa Nelson Mandela mjini Baraki, Algiers, Algeria.


Post a Comment (0)
Previous Post Next Post