YANGA YAOMBA MECHI NA SINGIDA IAHIRISHWE


UONGOZI wa Yanga SC umeandika barua Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuomba moja kati ya mechi zake mbili wiki hii ifutwe ili wapate muda kidogo wa kujiandaa na mechi dhidi ya Marumo Gallants Mei 10.
Yanga inakabiliwa na ratiba ngumu mno ya kucheza mechi tatu za mashindano tofauti ndani ya siku saba katika miji miwili, Singida na Dar es Salaam.
Alhamisi itakuwa mechi ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara na Jumapili Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) zote dhidi ya Singida Uwanja wa LITI.
Baada ya hapo watasafiri kurejea Dar es Salaam kwa mchezo wa kwanza wa Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Marumo Gallants ya Afrika Kusini Jumatano ijayo, Mei 10.
Na kikosi cha Yanga kimeondoka tena leo asubuhi kwenda Singida baada ya jana kwenda na kurudi kufuatia ndege kushindwa kutua kutokana na mazingira ya Uwanja wa Ndege.
Kwa mujibu wa ratiba ya Ligi Kuu, Yanga imebakiza jumla mechi nne za Ligi Kuu pamoja na huo wa Singida Big Stars, nyingine dhidi ya Dodoma Jiji, Mbeya City na Tanzania Prisons zote ugenini na wanatakiwa kushinda mechi tatu ili kuwa mabingwa tena.
Mechi ya marudiano na Marumo Gallants itafanyika Afrika Kusini Mei 17.


Post a Comment (0)
Previous Post Next Post